Tuesday, April 26, 2016

3,551 WASAMEHEWA


Rais John Magufuli ametoa msamaha kwa wafungwa 3,551, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 52 ya Muungano wa Tanzania.

Taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Meja Jenerali Projest Rwegasira ilisema wafungwa 580 wataachiwa huru, huku wengine 2,971 watapunguziwa moja ya sita ya vifungo vyao.
Alisema rais ametoa msamaha huo kwa kutumia madaraka aliyopewa chini ya ibara ya 45(1)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aliwataja watakaonufaika na msamaha huo kuwa ni wafungwa wenye ugonjwa wa ukimwi, kifua kikuu na saratani ambao wapo kwenye hatua za mwisho. Wengine ni wazee wenye umri wa miaka 70 na kuendelea, wajawazito na wale waliongia na watoto gerezani.
Wafungwa wengine watakaonufaika na msamaha huo ni wenye ulemavu wa akili ambao wamethibishwa na jopo la waganga kuwa wana tatizo hilo.
Katibu mkuu wa wizara hiyo alisema msamaha huo hautawagusa wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kunyongwa au kifungo cha maisha jela.
Pia, wafungwa wanaotumikia kifungo kwa makosa ya usafirishaji na matumizi ya dawa za kulevya, upokeaji na utoaji rushwa, matumizi mabaya ya madaraka, unyang’anyi kwa kutumia silaha na kubaka ni miongoni mwa waliokosa msamaha huo.
Wengine ambao hawataguswa na msamaha huo ni wale wanaotumikia vifungo kwa makosa ya kupatikana na  silaha, wizi wa magari na pikipiki, kuwapa mimba wanafunzi na ubadhirifu wa fedha za Serikali.
Wafungwa wengine watakaoendelea kubaki magerezani ni wale waliohukumiwa kutokana na usafirishaji wa nyara za Serikali na ujangili, utekaji wa watoto, biashara ya binadamu, kukutwa na viungo vya binadamu na waliojaribu kutoroka wakiwa chini ya ulinzi.
Katika maadhimisho ya Uhuru yaliyofanyika Desemba 9, 2015, Rais Magufuli aliwasamehe wafungwa 2,336, kati ya hao 117 waliachiwa huru huku 2,219 wakipunguziwa moja ya sita ya vifungo vyao.
Kwa idadi hiyo mpaka sasa wafungwa 5,887 wamenufaika na msamaha wa Rais Magufuli tangu aingie madarakani baada ya kushinda katika Uchaguzi Mkuu Oktoba 25, 2015.

Related Posts:

  • TWITTER YAMTIA NDANI MWANDISHI Polisi nchini Uturuki wamekamata mwandishi wa habari aliyemkosoa rais wa nchi hiyo kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter. Ebru Umar raia wa Uholanzi alikamatwa na polisi baada ya kumkosoa rais Recep Tayyip Erdogan alikamatwa… Read More
  • UGANDA: BOMBA LA MAFUTA KUPITIA TANZANIA Uganda imeamua kujenga bomba la mafuta yake kupitia Tanzania na wala sio Kenya. Awali taifa hilo la Afrika mashariki ambayo haijapakana na bahari ilikuwa imezungumzia nia ya kujenga bomba la mafuta yake kupitia Kenya lakini … Read More
  • BURIANI PAPA WEMBA Nyota wa muziki wa Soukous ambaye ni raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo- Papa Wemba amefariki dunia Papa Wemba ambaye jina lake halisi ni Jules Shungu Wembadio Pene Kikumba, alianguka na kufa jukwaani akiwatumbuiza ma… Read More
  • UKIMYA WA UPINZANI BUNGENI MASHAKA KWA WASOMI UAMUZI wa Kambi ya Upinzani bungeni kuingia katika vikao vya Bunge na kugeuka bubu wakati wa mjadala wa Hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, umechukuliwa kwa hadhari kuwa unaweza kusababisha kambi hiyo ionekane inalinda posho bu… Read More
  • Watumishi HEWA Wakopa Mamilioni ya Pesa Benki; Kilimanjaro Msako ulioanzishwa na Rais John Magufuli wa kutokomeza tatizo la wafanyakazi hewa katika utumishi wa umma, umeendelea kuibua mazito, ambapo mkoani Kilimanjaro, Benki ya CRDB imejikuta ikitoa mkopo kwa waliokuwa wafanya… Read More

0 comments:

Post a Comment