• This is Slide 1 Title

    This is slide 1 description. Go to Edit HTML and replace these sentences with your own words. This is a Blogger template by Lasantha - PremiumBloggerTemplates.com...

  • This is Slide 2 Title

    This is slide 2 description. Go to Edit HTML and replace these sentences with your own words. This is a Blogger template by Lasantha - PremiumBloggerTemplates.com...

  • This is Slide 3 Title

    This is slide 3 description. Go to Edit HTML and replace these sentences with your own words. This is a Blogger template by Lasantha - PremiumBloggerTemplates.com...

Friday, April 22, 2016

BOMBA LA MAFUTA KUPATA UAMUZI MWISHONI MWA WIKI

Viongozi wa Kenya, Uganda na Tanzania mwishoni mwa wiki wanatarajiwa kutoa uamuzi wa mwisho kuhusu ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Uganda na Kenya hadi pwani.

Mwaka jana, Kenya na Uganda zilikuwa zinashauriana kuhusu mpango wa kujenga bomba la kusafirisha mafuta kutoka Hoima, magharibi mwa Uganda, hadi bandari ya Lamu katika Pwani ya Kenya.

Bomba hilo la mafuta lilikusudiwa kutumiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka eneo la Ziwa Albert nchini Uganda na kutoka eneo lenye mafuta Kenya la Lokichar.

Rais Uhuru Kenyatta na Rais Yoweri Museveni walikutana nchini Uganda Agosti mwaka jana na kuafikiana kwamba ujenzi wa bomba hilo ulifaa kuharakishwa.

Lakini Rais wa Tanzania Dkt John Magufuli alikutana na Rais Museveni Machi mwaka huu na wawili hao wakakubaliana kuhusu mpango wa kujengwa kwa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Uganda hadi bandari ya Tanga katika pwani ya Tanzania.

Baadaye, Rais Magufuli alikutana na makamu wa rais wa kampuni ya Total Afrika Mashariki Bw Javier Rielo na wakaafikiana kwamba ujenzi wa bomba hilo linalokadiriwa kuwa la urefu wa kilomita 1,410 uanze haraka iwezekanavyo.

Kampuni ya mafuta ya Total ndiyo inayofadhili ujenzi huo.

Bw Javier alisema kampuni yake inatarajia kutumia dola za kimarekani karibu bilioni 4 ambazo tayari zimeshaandaliwa.

SERIKALI YAPONGEZWA NA SHIRIKISHO LA WAFANYAKAZI ZANZIBAR

SHIRIKISHO la Vyama Huru vya Wafanyakazi Zanzibar (ZATUC) limeelezea kuridhishwa na juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kutekeleza mapendekezo yake, ikiwemo kuundwa kwa chombo cha majadiliano kitaifa chenye lengo la kuleta ufanisi sehemu za kazi na kuondoa migogoro.

Katibu Mkuu wa ZATUC, Khamis Mwinyi alisema hayo jana wakati akizungumza na gazeti hili kuhusu mafanikio na changamoto zinazowakabili wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta binafsi.

Mwinyi alisema kitendo cha Serikali ya Mapinduzi kukubali kuundwa kwa chombo hicho na kuanza kutekeleza majukumu yake kwa kiasi kikubwa kitasaidia kuleta ufanisi sehemu za kazi na kuondoa malumbano ambayo yamekuwa yakijitokeza baina ya Serikali na Shirikisho hilo kuhusu maslahi na stahili za wafanyakazi nchini.

“Tunaipongeza Serikali hii kukubali kuunda chombo cha majadiliano kitaifa ambacho kimekuwa kilio chetu kwa muda mrefu,” alisema.

Akifafanua, Mwinyi alisema chombo cha majadiliano na Serikali kinaundwa na wajumbe 10 kutoka Serikalini na vyama vya wafanyakazi na Mwenyekiti wake ni Naibu Katibu Mkuu Baraza la Mapinduzi pamoja na wajumbe wengine kutoka katika ZATUC.

Alisema tayari vikao mbalimbali vimefanyika kwa mujibu wa kalenda ambavyo vimesaidia kwa kiasi kikubwa kuzipitia changamoto mbalimbali zilizopo na kupatiwa ufumbuzi.

Aidha Mwinyi alisema tayari Mahakama ya Kazi imeanza kusikiliza kesi mbalimbali zinazohusu wafanyakazi wa sekta mbalimbali na kutolewa hukumu, hatua ambayo imesaidia kuondoa mlundikano wa mashauri ya malalamiko.

Alisema hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya Shirikisho la Vyama Huru vya Wafanyakazi kwa sababu itasaidia kutoa haki kwa wafanyakazi kuweza kusikilizwa mashauri yao mbele ya mahakama na hivyo kuimarisha ufanisi na uzalishaji sehemu za kazi.

Hata hivyo, Mwinyi alisema wafanyakazi wa Zanzibar ikiwemo wa sekta binafsi na serikali wanakabiliwa na changamoto kubwa ambazo zinahitaji kupatiwa ufumbuzi haraka.

Alitaja moja ya changamoto hizo ombi la kutaka kima cha chini cha mishahara kwa wafanyakazi wa Serikali kupanda zaidi kutoka cha sasa cha Sh 150,000 na sekta binafsi Sh 145,000.

Alisema viwango hivyo vimepitwa sana wakati. Alisema mwaka 2000 shirikisho hilo lilitafuta mshauri mwelekezi kwa ajili ya kufanya utafiti kuhusu kiwango cha mishahara ambapo utafiti huo ulikamilika mwaka 2011 na kuonesha kwamba kiwango cha chini kwa wafanyakazi wa serikali kilipaswa kuwa Sh 350,000.

Alitaja changamoto nyingine zinazowakabili wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa ni tofauti ya mishahara kutoka kwa wenzao walio katika serikali ya Muungano, tofauti ambayo ni kubwa wakati wote ingawa wanatumia soko moja la bidhaa.

MADAWA HARAMU, E.P.L

Serikali ya Uingereza imeanzisha uchunguzi wa dharura kufuatia ufichuzi kuwa wachezaji nyota wa kandanda nchini Uingereza wamekuwa wakitumia madawa yaliyopigwa marufuku ya kuongeza nguvu mwilini.

Gazeti la Sunday Times limechapisha ripoti ya uchunguzi iliyothibitisha kuwa sio tu wasakataji dimba bali hata waendesha baiskeli, wachezaji Kriketi na hata wachezaji wa tenisi wamekuwa wakipokea matibabu kutoka kwa daktari mmoja ambaye anajulikana kwa kupeana madawa hayo yaliyopigwa marufuku ya kututumua misuli.

Daktari Mark Bonar ambaye anazahanati yake mjini London Uingereza amekuwa akiwatoza wachezaji nyota maelfu ya pauni za Uingereza kwa matibabu hayo fiche ambayo imegunduliwa kuwa ni matibabu ya madawa yaliyopigwa marufuku na shirikisho la kupambana na madawa haramu WADA.

Wateja wakuu wa Dkt Bonar yasemekana ni wachezaji wa timu kuu katika ligi maarufu zaidi duniani ligi ya Uingereza.

Uchunguzi pia umebaini kuwa dkt Bonar amekuwa akiwapa wachezaji nyota 150 dawa aina ya EPO Steroids na hata homoni zinazokua kwa haraka ambazo ni haramu katika michezo katika kipindi cha miaka 6 sasa.

Serikali ya Uingereza imeanzisha uchunguzi dhidi ya taasisi ya kupambana na kuenea kwa madawa hayo haramu kufuatia ufichuzi huo.

Hakuna ushahidi kuwa timu za ligi kuu ya Uingereza zilifahamu mbinu za dkt Bonar.

Image copyrightGettyImage captiondkt Bonar amekuwa akiwapa wachezaji nyota 150 dawa aina ya EPO Steroids na hata homoni zinazokua kwa haraka

Aidha Sunday Times linasema kuwa halina ushahidi 'huru' kuwa dkt Bonar aliwapa madawa hayo ya kututumua misuli wachezaji wangapi wanaochezea vilabu vya ligi kuu ya Uingereza EPL.

Hata hivyo wachezaji kadhaa walioulizwa iwapo walipewa madawa hayo ya kututumua misuli na dkt Bonar walikataa kujibu na wengine wakakanusha madai hayo ya daktari huyo.

Dkt Bonar hata hivyo anasema kuwa hakuwapa wachezaji hao madawa hayo kwa nia ya kuimarisha uwezo wao uwanjani ila anadai aliwapa madawa hayo ilikuwatibu dhidi ya maradhi mbali mbali waliokuwa wanaugua.

Uchunguzi huu unatokana na ufichuzi wa mchezaji mmoja aliyekwenda kwa idara ya serikali kumshtaki dkt Bonar kwa kumpa dawa iliyopigwa marufuku.

Mchezaji huyo ambaye ametaka jina lake libanwe anasema alipigwa na butwaa dkt Bonar aliposisitiza kuwa anastahili kumeza dawa hiyo haramu.

Sunday Times lilitumia mwanariadha chipukizi kumrekodi daktari huyo akijigamba jinsi alivyowatibu wachezaji wengi tu nyota akitumia mbinu zizo hizo japo ni marufuku.

WAPENZI JINSIA MOJA WATAHADHARISHWA UK

Serikali ya Uingereza imewaonya wapenzi wa jinsia moja wanaosafiri kuelekea Marekani kutokana na sheria dhidi yao katika majimbo ya North Carolina and Mississippi.

Marekani ni jamii kubwa ilio na maoni tofauti.Sheria mpya zilizopitishwa katika majimbo hayo zinaruhusu wafanyibiashara kuamua iwapo wanaweza kuwahudumia watu wa jinsia hiyo au la.

Ushauri huo umetoka katika afisi ya maswala ya kigeni ya Uingereza.

Katika jimbo la Carolina,sheria iliopitishwa na Gavana Pat McCrory inasema kuwa watu waliobadili jinsia watumie msaala wa kuogea kulingana na jinsia yao iliopo katika vyeti vyao vya kuzaliwa.

Sheria ya Mississippi pia ina sheria kama hiyo na inawalinda wafanyibiashara wengi kytoshtakiwa kwa kukataa kuwauzia wapenzi wa jinsia moja.

KANYE ASHTAKIWA KWA ULAGHAI

Shabiki mmoja ameamua kumshtaki nyota wa muziki wa Rap Kanye West pamoja na huduma ya muziki ya Tidal kuhusu kutolewa kwa albamu mpya ya mwanamuziki huyo,The life of Pablo.

Justin Baker-Rhett anadai alidanganywa kutia saini na kujiunga na huduma hiyo ya moja kwa moja,kwa kuwa ilikuwa njia ya pekee ya kununua albamu hiyo ya West.

Alisema kuwa alijiunga na Tidal baada ya mwanamuziki huyo kusema kuwa albamu yake haitauzwa mahali pengine.

Na sasa anasema kuwa hatua hiyo ni ya kilaghai na ililenga kuipatia Tidal mamilioni ya wateja.

Kanye West alitoa albamu yake mwezi mmoja baadaye katika Apple Muzic,Spotify pamoja na katika mtandao wake.

Baker Rhet anasema kuwa hatua hiyo iliiongezea wateja Tidal mara tatu na kupiga jeki thamani yake kufikia dola milioni 84.

REFA MAREHEMU KUAMUA MECHI

Mwanamume aliyefariki ameteuliwa kusimamia mechi ya soka nchini Nigeria ambayo itachezwa Jumapili, mwandishi wa BBC anayefuatilia masuala ya soka Oluwashina Okeleji anasema.

Wale Akinsanya aliteuliwa kuwa mwamuzi kwenye mechi baina ya Warri Wolves na Giwa FC katika mji wa Warri kusini mwa Nigeria, gazeti la Punch la Nigeria limeripoti.

Hii ni licha ya kwamba Akinsanya alifariki tarehe 22 Januari 2016 wakati wa kufanywa kwa mtihani wa Fifa Cooper Test, ambao hutumiwa kuamua iwapo marefarii wanatosha kuendelea kusimamia mechi.

DONALD TRUMP AAHIDI KUJIBADILISHIA SIFA

Mgombea wa urais nchini Marekani kwa tiketi ya chama cha Republican Donald Trump ameahidi kubadilisha sifa zake katika mkutano wa faragha na viongozi wa Republican.

Mfanyibishara huyo ambaye yuko kifua mbele katika kuwania urais kupitia chama hicho alitoa ujumbe wake kupitia wasaidizi wake ,kulingana na chombo cha habari cha AP.

Kuimarika kwake katika mchujo huo kufikia sasa kumetuma ishara miongoni mwa viongozi wa chama hicho kwamba matamshi pamoja na sera zake huenda zisiwavutie wapiga kura.

Majimbo matano yanapiga kura siku ya Jumanne kumchagua mgombea wao wa urais.

Bwana Trump ana uongozi mkubwa wa idadi ya wajumbe lakini huenda asipate wajumbe 1,237 anaohitaji kushinda mchujo huo bila ya mkutano wa wanachama.

Wasaidizi wamewaambia viongozi wa chama kwamba amekuwa akibadilisha sifa zake na kwamba hatua hiyo imeanza kufua dafu.

MAJAMBAZI WAUA KWENYE TUKIO LA UPORAJI SUPPERMARKET

WAKAZI wanne wa jijini Tanga wamekufa papo hapo na wengine wawili kujeruhiwa kwa risasi na majambazi .

Majambazi hao waliokuwa na bunduki aina ya SMG , walivamia juzi duka kuu (supermarket) la mfanyabiashara Hamoud Ali lililopo Mtaa wa Swahili katika kata ya Central jijini Tanga .

Waliokufa katika tukio hilo ni Ahmed John, Vitus Manfred ambaye ni dereva wa gari la Mahakama ya Hakimu Mkazi Tanga, Athumani Seya pamoja na Ali Mpemba ambaye ni mfanyakazi kwenye duka hilo.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Leonard Paul tukio hilo ni la juzi saa 1.30 usiku.

‘’Wakati biashara inaendelea ndani ya hilo duka kuu , ghafla waliingia watu wengine zaidi kama wateja ambao baada ya muda mfupi walibadilika na kutoa silaha za moto”, alisema.

Aliongeza “Kitendo chao hicho kilienda sambamba na amri ya kuwataka watu wote waliokuwa humo dukani kulala chini ambapo inadaiwa walitii na kisha wakaamua kuwapiga risasi maeneo ya kichwani wateja wanne waliokuwemo.”

Kamanda alisema majambazi hao walipora Sh milioni 2.7 na kukimbilia kusikojulikana.